Page 24 - Kiswahili Grade 5 Yaliyomo ya kidijitali
P. 24
6. Maadili
Mlango 12. Kisa cha Sungura na Nyani
Mlango 13. Kosa Langu Mjini
Kusikiliza na kuzungumza
Shairi 1
Wahuni wa kijijini
Waliishi hapo zama, wahuni wa kijijini,
Waliishi kwa zahama, mfano wa mahaini,
Hawakuwa na huruma, hata tone vifuani,
Na maadili daima, walitupa jalalani.
Hawakuwa na heshima, kwa yeyote asilani,
Matukano yalivuma, kote kote kijijini,
Hata haki walinyima, wanyama wa mazizini,
Na maadili daima, walitupa jalalani.
Usawa walisukuma, na kuutupa topeni,
Uwajibikaji nyuma, ukishika mkiani,
Uadilifu waama, ulibaki neno geni,
Na maadili daima, walitupa jalalani.
Walianza kujiuma, kwa majuto vidoleni,
Kwa huzuni wakasema, watauacha uhuni,
Waligundua zahama, daima ni uhaini,
Na maadili daima, wakatia maanani.
Ilitimu siku njema, akaja mtu kayani,
Pembe zote akasema, huna faida uhuni,
Watoto hata wazima, mafunzo wakaamini,
Na maadili daima, wakatia maanani.